Alhamisi, 27 Septemba 2018

Uchaguzi Kutoka katika Mafungu Kumi ya Neno la Mungu juu ya "Kuhusu Biblia"

Mwenyezi Mungu, Biblia, Bwana Yesu,

Uchaguzi Kutoka katika Mafungu Kumi ya Neno la Mungu juu ya "Kuhusu Biblia"

1. Kwa miaka mingi, imani ya watu ya kitamaduni (hiyo ya Ukristo, moja ya dini kuu tatu za dunia) imekuwa ni kusoma Biblia; kujitenga na Biblia sio imani kwa Bwana, kujitenga na Biblia ni madhehebu maovu, na uzushi, na hata pale watu wanaposoma vitabu vingine, msingi wa vitabu hivi ni lazima uwe ni ufafanuzi wa Biblia. Ni kusema kwamba, kama unasema unamwamini Bwana, basi ni lazima usome Biblia, unapaswa kula na kunywa Biblia, na nje ya Biblia hupaswi kuabudu kitabu kingine ambacho hakihusishi Biblia. Ikiwa utafanya hivyo, basi unamsaliti Mungu. Kuanzia kipindi ambapo kulikuwa na Biblia, imani ya watu kwa Bwana imekuwa imani katika Biblia. Badala ya kusema watu wanamwamini Bwana, ni bora kusema kwamba wanaamini Biblia; badala ya kusema wameanza kusoma Biblia, ni bora kusema wameanza kuamini Biblia; na badala ya kusema wamerudi mbele ya Bwana, ingekuwa vyema kusema wamerudi mbele ya Biblia. Kwa njia hii, watu wanaiabudu Biblia kana kwamba ni Mungu, kana kwamba ni damu yao ya uzima na kuipoteza itakuwa ni sawa na kupoteza maisha yao. Watu wanaitazama Biblia kuwa ni kuu kama Mungu, na hata kuna wale wanaoiona kuwa ni kuu kuliko Mungu. Kama watu hawatakuwa na kazi ya Roho Mtakatifu, ikiwa hawawezi kuhisi Mungu, wanaweza kuendelea kuishi—lakini punde tu watakapoipoteza Biblia, au kupoteza sura na maneno maarufu sana kutoka katika Biblia, basi inakuwa ni kana kwamba wamepoteza maisha yao. Na hivyo, pale ambapo watu wataanza kumwamini Bwana wanaanza kusoma Biblia, na kuikariri Biblia, na kadri ya sehemu kubwa ya Biblia wanayoweza kukariri, ndivyo hii inathibitisha kwamba wanampenda Bwana na ni watu wenye imani kuu. Wale ambao wameisoma Biblia na wanaweza kuizungumzia kwa wengine wote ni kaka na dada wazuri. Kwa miaka yote hii, imani ya watu na uaminifu kwa Bwana vimepimwa kulingana na kiwango cha ufahamu wao wa Biblia. Watu wengi hawaelewi kwa nini wanapaswa kumwamini Mungu, wala jinsi ya kumwamini Mungu, na hawafanyi chochote zaidi ya kutafuta kiupofu dondoo ili kufasiri sura za Biblia. Hawajawahi kufuata mwelekeo wa kazi ya Roho Mtakatifu; muda wote huo, hawajafanya chochote, bali kujifunza na kuchunguza Biblia kwa papara, na hakuna hata mmoja ambaye amepata kazi mpya ya Roho Mtakatifu nje ya Biblia, hakuna ambaye amewahi kujitenga na Biblia, wala kuthubutu kujitenga na Biblia. Watu wamejifunza Biblia kwa miaka yote hii, wamekuja na maelezo mengi sana, na kufanya kazi kubwa sana, pia wana maoni mengi tofauti kuhusu Biblia, ambayo yamekuwa ni mdahalo usiokwisha, kiasi kwamba ziadi ya madhehebu elfu mbili yameanzishwa hadi leo. Wote wanataka kutafuta ufafanuzi maalumu, au siri za kina zaidi katika Biblia, wanataka kuichunguza, na kuipata katika usuli wa kazi ya Yehova katika Israeli, au usuli wa kazi ya Yesu katika Yudea, au siri nyingi zaidi ambazo hakuna yeyote anayejua. Watu wanavyoichukulia Biblia ni shauku na imani, na hakuna anayeweza kufafanua kikamilifu kisa cha ndani au kiini cha Biblia. Hivyo, matokeo yake ni kwamba leo, watu bado wana hisia zisizoelezeka za kimiujiza linapokuja suala la Biblia; hata zaidi ya hapo, wana shauku nayo sana, na wanaiamini. Leo, kila mtu anataka kutafuta unabii wa kazi ya siku za mwisho katika Biblia, wanataka kugundua ni kazi gani Mungu hufanya wakati wa siku za mwisho na kuna ishara gani ya siku za mwisho. Kwa njia hii, kuabudu kwao Biblia kunakuwa na maana sana, na kadri wanaposogelea siku za mwisho, ndivyo wanavyozidi kuonyesha imani kwenye unabii wa Biblia, hususani ule wa siku za mwisho. Kwa imani hiyo ya upofu katika Biblia, kwa imani hiyo katika Biblia, hawana shauku ya kutafuta kazi ya Roho Mtakatifu. Katika dhana za watu, wanadhani kwamba ni Biblia pekee ndiyo inayoweza kuleta kazi ya Roho Mtakatifu; ni katika Biblia pekee ndimo wanamoweza kupata nyayo za Mungu; ni katika Biblia pekee ndimo kulimofichika siri za kazi ya Mungu; ni kwenye Biblia pekee—na sio katika vitabu vinginevyo au watu—wanaoweza kufafanua kila kitu cha Mungu na ujumla wa kazi Yake; Biblia inaweza kuleta kazi ya mbinguni duniani; na Biblia inaweza kuanzisha na kuhitimisha enzi. Kwa dhana hizi, watu hawana shauku kutafuta kazi ya Roho Mtakatifu. Hivyo, licha ya kiasi gani Biblia ilikuwa ina msaada mkubwa kwa watu wa wakati wa nyuma, imekuwa ni kikwazo katika kazi ya Mungu ya hivi karibuni. Bila Biblia, watu wanaweza kutafuta nyayo za Mungu mahali kwingineko, bado leo, nyayo zake zimejumuishwa na Biblia, na kupanua kazi Yake ya hivi karibuni, imekuwa na ugumu mara mbili, na mapambano magumu. Hii yote ni kwa sababu ya sura na misemo maarufu kutoka katika Biblia, vilevile unabii mbalimbali wa Biblia. Biblia imekuwa sanamu katika akili za watu, limekuwa ni fumbo katika akili zao, na hawawezi kabisa kuamini kwamba Mungu anaweza kufanya kazi nje ya Biblia, hawawezi kuamini kwamba watu wanaweza kumpata Mungu nje ya Biblia, achilia mbali kuwa na uwezo wa kuamini kwamba Mungu angeweza kujitenga na Biblia wakati wa kazi ya mwisho na kuanza upya. Hili suala haliingii akilini mwa watu; hawawezi kuliamini, na wala hawawezi kulifikiria. Biblia imekuwa kikwazo kikubwa kwa watu kukubali kazi mpya ya Mungu, na imefanya kuwa vigumu kuipanua kazi hii mpya.
kutoka kwa "Kuhusu Biblia (1)" katika Neno Laonekana katika Mwili
2. Nyakati za kale, kabla ya Enzi za Neema watu walisoma Biblia, lakini wakati huo kulikuwa na Agano la Kale tu; hakukuwa na Agano Jipya. Kwa kuwa kulikuwa na Agano la Kale la Biblia, watu walianza kusoma maandiko matakatifu. Baada ya kuongozwa kwake na Yehova kukamilika, Musa aliandika Mwanzo, Kutoka, na Kumbukumbu la Torati.... Alikumbuka kazi ya Yehova wakati huo, na akaiandika. Biblia ni kitabu cha historia. Ni kweli, pia kinahusisha baadhi ya unabii wa manabii, na ni kweli, unabii huu, kwa namna yoyote ile si historia. Biblia inajumuisha sehemu kadhaa—sio unabii tu, au kazi ya Yehova tu, wala hakuna nyaraka za Paulo pekee. Unapaswa kujua ni sehemu ngapi ambazo Biblia inajumuisha; Agano la Kale linajumuisha Mwanzo, Kutoka..., na pia kuna vitabu vya unabii ambavyo waliandika. Mwishoni, Agano la Kale linakamilika kwa kitabu cha Malaki. Linarekodi kazi ya Enzi ya Sheria, ambayo iliongozwa na Yehova; kuanzia Mwanzo hadi Kitabu cha Malaki, ni rekodi kamilifu ya kazi ya Enzi ya Sheria. Ni sawa na kusema, Agano Jipya linarekodi yote ambayo yalipitiwa na watu ambao waliongozwa na Yehova katika Enzi ya Sheria. Wakati wa Enzi ya Sheria ya Agano la Kale, idadi kubwa ya manabii iliinuliwa na Yehova, walizungumza unabii kwa niaba Yake, walitoa maelekezo kwa makabila mbalimbali na mataifa, na wakatoa unabii juu ya kazi ambayo Yehova angefanya. Watu hawa ambao wameinuliwa wote walipewa na Yehova Roho ya unabii: Waliweza kutazama njozi kutoka kwa Yehova, na kusikia sauti Yake, na hivyo walivuviwa Naye na wakaandika unabii. Kazi waliyoifanya ilikuwa udhihirisho wa sauti ya Yehova, ilikuwa ni kazi ya unabii ambayo waliifanya kwa niaba ya Yehova, na kazi ya Yehova wakati huo ilikuwa ni kuwaongoza watu kwa njia ya Roho Mtakatifu; Hakufanyika mwili, na watu hawakuona uso Wake. Hivyo, aliwainua manabii wengi kufanya kazi Yake, na akawapatia mashauri ambayo waliyapelekea katika kila kabila na ukoo wa Israeli. Kazi yao ilikuwa ni kusema unabii, na baadhi yao waliandika maelekezo ya Yehova kwa ajili yao ili kuwaonesha wengine. Yehova aliwainua watu hawa kuzungumza unabii, kutoa unabii wa kazi ya wakati ujao au kazi ambayo ilikuwa bado haijafanyika wakati huo, ili kwamba watu wangeweza kutazama maajabu na hekima ya Yehova. Vitabu hivi vya unabii vilikuwa tofauti kabisa na vitabu vingine vya Biblia; yalikuwa ni maneno yaliyozungumzwa au kuandikwa na wale waliopewa Roho ya unabii—na wale ambao walipata njozi au sauti kutoka kwa Yehova. Kuacha vitabu vya unabii, kila kitu kingine katika Agano la Kale ni rekodi zilizochukuliwa na watu baada ya Yehova kukamilisha kazi Yake. Vitabu hivi haviwezi kusimama badala ya unabii uliozungumzwa na manabii walioinuliwa na Yehova, kama ambavyo Mwanzo na Kutoka haviwezi kulinganishwa na Kitabu cha Isaya na Kitabu cha Danieli. Unabii ulikuwa unazungumzwa kabla ya kazi haijafanyika; wakati huo, vitabu vingine viliandikwa baada ya kuwa kazi imemalizika, kazi ambayo watu walikuwa wanaiweza. … Kwa namna hii, kile kilichorekodiwa katika Biblia ni kazi katika Israeli pekee wakati huo. Maneno yaliyozungumzwa na manabii, na Isaya, Danieli, Yeremia na Ezekieli ... maneno yao yanatabiri kazi Yake nyingine duniani, yanatabiri kazi ya Yehova Mungu Mwenyewe. Yote haya yalitoka kwa Mungu, ilikuwa ni kazi ya Roho Mtakatifu, na tofauti na vitabu hivi vya manabii, mambo mengine yote ni rekodi ya uzoefu wa watu juu ya kazi ya Yehova wakati huo.
kutoka kwa "Kuhusu Biblia (1)" katika Neno Laonekana katika Mwili
3. Kazi ya uumbaji ilitokea kabla ya binadamu kuwepo, lakini Kitabu cha Mwanzo kilikuja tu baada ya kuwepo binadamu; kilikuwa ni kitabu kilichoandikwa na Musa wakati wa Enzi ya Sheria. Ni kama vitu vilivyotokea miongoni mwenu leo: Baada ya kutokea, mnayaandika ili kuwaonyesha watu katika maisha ya baadaye, na kwa watu wa baadaye, mliyoyarekodi ni mambo yaliyotokea wakati uliopita—na si chochote zaidi ya historia. Mambo yaliyorekodiwa katika Agano la Kale ni kazi ya Yehova katika Israeli, na kile kilichorekodiwa katika Agano Jipya ni kazi ya Yesu katika Enzi ya Neema; ni rekodi ya kazi iliyofanywa na Mungu katika enzi mbili tofauti. Agano la Kale linarekodi kazi ya Mungu wakati wa Enzi ya Sheria, na hivyo Agano la Kale ni kitabu cha kihistoria, wakati Agano Jipya ni zao la kazi ya Enzi ya Neema. Wakati kazi mpya ilipoanza, vitabu hivi vilipitwa na wakati—na hivyo, Agano Jipya pia ni kitabu cha kihistoria. Kimsingi Agano Jipya halina mpangilio mzuri kama Agano la Kale, wala halirekodi mambo mengi.
kutoka kwa "Kuhusu Biblia (1)" katika Neno Laonekana katika Mwili
4. Biblia ni kitabu cha aina gani? Agano la Kale ni kazi ya Mungu katika Enzi ya Sheria. Agano la Kale la Biblia linarekodi kazi yote ya Yehova wakati wa Enzi ya Sheria na kazi Yake ya uumbaji. Lote linarekodi kazi iliyofanywa na Yehova, na hatimaye linahitimisha maelezo ya kazi ya Yehova kwa kitabu cha Malaki. Agano la Kale linarekodi kazi mbili zilizofanywa na Mungu: Moja ni kazi ya uumbaji, na nyingine ni kuamrisha sheria. Zote ni kazi zilizofanywa na Yehova. Enzi ya Sheria inawakilisha kazi ya Mungu chini ya jina la Yehova; ni ujumla wa kazi iliyofanywa kimsingi chini ya jina la Yehova. Hivyo, Agano la Kale linarekodi kazi ya Yehova, na Agano Jipya linarekodi kazi ya Yesu, kazi ambayo kimsingi ilifanywa chini ya jina la Yesu. Umuhimu mkubwa wa jina la Yesu na kazi Aliyoifanya imerekodiwa katika Agano Jipya.
kutoka kwa "Kuhusu Biblia (1)" katika Neno Laonekana katika Mwili
5. Ikiwa unatamani kuiona kazi ya Enzi ya Sheria, na kuona jinsi gani Waisraeli waliifuata njia ya Yehova, basi ni lazima usome Agano la Kale; ikiwa unatamani kuelewa kazi ya Enzi ya Neema, basi ni lazima usome Agano Jipya. Lakini unawezaje kuona kazi ya siku za mwisho? Ni lazima ukubali uongozi wa Mungu wa leo, na kuingia katika kazi ya leo, maana hii ni kazi mpya na hakuna ambaye ameirekodi katika Biblia hapo nyuma. Leo, Mungu amefanyika mwili, na Amewachagua wateule wengine katika nchi ya China. Mungu anafanya kazi ndani ya watu hawa, Anaendelea na kazi Yake duniani, Anaendelea kutoka katika kazi ya Enzi ya Neema. Kazi ya leo ni njia ambayo mwanadamu hajawahi kuiendea, na njia ambayo hakuna mtu ambaye amewahi kuiona. Ni kazi ambayo haijawahi kufanywa hapo kabla—ni kazi ya Mungu ya hivi karibuni kabisa duniani. Hivyo, kazi ambayo haijawahi kufanywa kabla sio historia, kwa sababu sasa ni sasa, na bado haijawa muda uliopita. Watu hawajui kwamba Mungu amefanya kazi kubwa, mpya duniani, na nje ya Israeli, yaani imevuka mawanda ya Israeli, na zaidi ya unabii wa manabii, ambayo ni kazi mpya na ya kushangaza nje ya unabii, na kazi mpya kabisa nje ya Israeli, na kazi ambayo watu hawawezi kuielewa au kufikiria. Inawezekanaje Biblia kuwa na rekodi za wazi za kazi kama hiyo? Ni nani ambaye angeweza kurekodi kila hatua ya kazi ya leo, bila kuondoa kitu? Ni nani angeweza kurekodi kazi hii kubwa na yenye hekima ambayo inakataa maagano ya kitabu cha kale? Kazi ya leo sio historia, na kama vile, ikiwa unatamani kutembea katika njia ya leo, basi mnapaswa kutengana na Biblia, unapaswa kwenda mbele zaidi ya vitabu vya unabii au historia ya Biblia. Baada ya hapo tu ndipo utaweza kutembea njia mpya vizuri, na baada ya hapo ndipo utaweza kuingia katika ufalme mpya na kazi mpya. Unapaswa kuelewa ni kwa nini leo unaambiwa usisome Biblia, kwa nini kuna kazi nyingine ambayo inajitenga na Biblia, kwa nini Mungu haonekani mpya na wa kina zaidi katika Biblia, kwa nini badala yake kuna kazi kubwa zaidi nje ya Biblia. Haya ndiyo yote mnayopaswa kuelewa. Unapaswa kuelewa tofauti kati ya kazi ya zamani na kazi mpya, na hata kama hausomi Biblia, unapaswa kuitenganisha; kama hautaweza, bado utakuwa unaiabudu Biblia, na itakuwa ni vigumu sana kwako kuingia katika kazi mpya na kupitia mabadiliko mapya.
kutoka kwa "Kuhusu Biblia (1)" katika Neno Laonekana katika Mwili
6. Kwa kuwa kuna njia ya juu, kwa nini mjifunze hiyo ya chini, njia ya kale? Kwa kuwa kuna matamshi mapya, na kazi mpya, kwa nini uishi katikati ya rekodi za kale za kihistoria? Matamshi mapya yanaweza kukupa, ambayo yanathibitisha kwamba hii ni kazi mpya; rekodi za kale haziwezi kukushibisha, au kutosheleza mahitaji yako ya sasa, kitu ambacho kinathibitisha kwamba ni historia, na sio kazi ya hapa na sasa. Njia ya juu zaidi ni njia mpya zaidi, na kazi mpya, bila kujali njia ya zamani ni ya juu kiasi gani, bado ni historia ya kumbukumbu ya watu, na haijalishi ina thamani kiasi gani kama rejeleo, bado ni njia ya kale. Ingawa imerekodiwa katika "kitabu kitakatifu," njia ya kale ni historia; ingawa hakuna rekodi yake katika "kitabu kitakatifu," njia mpya ni ya hapa na sasa. Kwa njia hii inaweza kukuokoa, na kwa njia hii inaweza kukubadilisha, maana hii ni kazi ya Roho Mtakatifu.
kutoka kwa "Kuhusu Biblia (1)" katika Neno Laonekana katika Mwili
7. Biblia ni kitabu cha kihistoria, na ikiwa ungekula na kunywa Agano la Kale wakati wa Enzi ya Neema—ikiwa ungeweka katika vitendo kile kilichokuwa kinatakiwa katika wakati wa Agano la Kale wakati wa Enzi ya Neema—Yesu angekukataa, na kukuhukumu; ikiwa ungetumia Agano la Kale katika kazi ya Yesu, basi ungekuwa Farisayo. Ikiwa, leo, utaweka pamoja Agano Jipya na la Kale kula na kunywa, na kuliweka katika vitendo, basi Mungu wa leo Atakuhukumu; utakuwa umetanga mbali na kazi ya Roho Mtakatifu leo! Ikiwa unakula Agano la Kale, na kula Agano Jipya, basi upo nje ya mkondo wa Roho Mtakatifu! Wakati wa kipindi cha Yesu, Yesu aliwaongoza Wayahudi na wale wote ambao walimfuata Yeye kulingana na kazi ya Roho Mtakatifu katika Yeye wakati huo. Hakuichukulia Biblia kama msingi wa kile Alichofanya, bali Alizungumza kulingana na kazi Yake; Hakutilia maanani kile ambacho Biblia ilisema, wala hakutafuta katika Biblia njia ya kuongoza wafuasi Wake. Kuanzia pale Alipoanza kufanya kazi, Aliongoza njia ya toba—neno ambalo halikutajwa kabisa katika unabii wa Agano la Kale. Sio kwamba tu Hakutenda kulingana na Biblia, lakini pia Aliongoza njia mpya, na Akafanya kazi mpya. Na wala Hakurejelea kabisa Biblia Alipohubiri. Wakati wa Enzi ya Sheria, hakuna ambaye aliweza kufanya miujiza Yake ya kuponya wagonjwa na kutoa mapepo. Kazi Yake, mafundisho Yake, mamlaka Yake—hakuna mtu aliyefanya hivi wakati wa Enzi ya Sheria. Yesu alifanya tu kazi Yake mpya, na ingawa watu wengi walimhukumu kwa kutumia Biblia—na hata wakatumia Agano la Kale kumsulubisha—kazi Yake ilipitiliza Agano la Kale; kama hii haikuwa hivyo, kwa nini watu walimwangika msalabani? Ilikuwa ni kwa sababu haikusema kitu katika Agano la Kale la mafundisho Yake, na uwezo Wake wa kuponya wagonjwa na kutoa mapepo? Kazi Yake ilikuwa ni kwa ajili ya kuongoza katika njia mpya, haikuwa ni kwa makusudi ya kufanya ugomvi dhidi ya Biblia, au kwa makusudi kujitenga na Agano la Kale. Alikuja tu kufanya huduma Yake, kuleta kazi mpya kwa wale waliomtamani sana na kumtafuta. Hakuja kufafanua Agano la Kale au kutetea kazi yake. Kazi Yake bado haikuwa ni kwa ajili ya kuruhusu Enzi ya Sheria kuendelea kukua, maana kazi Yake haikuzingatia Biblia kama msingi wake; Yesu alikuja kufanya tu kazi ambayo Alipaswa kufanya. Hivyo, Hakufafanua unabii wa Agano la Kale, wala Hakufanya kazi kulingana na maneno ya Enzi ya Sheria ya Agano la Kale. Alipuuzia kile ambacho Agano la Kale lilisema, Hakujalia kama lilikubaliana na kazi Yake au la, na Hakujali kile ambacho watu wengine walijua kuhusu kazi Yake, au namna walivyokuwa wakiihukumu. Aliendelea tu kufanya kazi ambayo Alipaswa kufanya, ingawa watu wengi walitumia unabii waliousema manabii wa Agano la Kale kumhukumu. Ilionekana kwa watu kana kwamba kazi Yake haikuwa na msingi, na kulikuwa na mengi ambayo yalikuwa hayapatani na rekodi za Agano la Kale. Je, huu sio upuuzi? Je, kuna ulazima wa kutumia mafundisho ya dini katika kazi ya Mungu? Je, ni lazima iwe kulingana na maneno ya unabii waliyosema manabii? Hata hivyo, kipi ni kikubwa? Mungu au Biblia? Kwa nini ni lazima kazi ya Mungu iwe kulingana na Biblia? Je, inaweza kuwa kwamba Mungu hana haki ya kuwa juu ya Biblia? Je, Mungu hawezi kujitenga na Biblia na kufanya kazi nyingine? Kwa nini Yesu na wanafunzi Wake hawakutunza Sabato? Ikiwa Angetunza Sabato na matendo mengine kulingana na amri za Agano la Kale, kwa nini Yesu Hakutunza Sabato baada ya kuja, lakini badala yake Aliitawadha miguu, Alivunja mkate, na kunywa divai? Je, sio kwamba haya yote hayapatikani katika amri za Agano la Kale? Ikiwa Yesu aliliheshimu Agano la Kale, kwa nini Aliyakataa mafundisho haya. Unapaswa kujua ni kipi kilitangulia, Mungu au Biblia! Kuwa Bwana wa Sabato, je, Asingeweza pia kuwa Bwana wa Biblia?
kutoka kwa "Kuhusu Biblia (1)" katika Neno Laonekana katika Mwili
8. Biblia pia huitwa Agano la Kale na Agano Jipya. Je, mnajua "agano" linarejelea nini? "Agano" katika Agano la Kale linatokana na makubaliano ya Yehova na watu wa Israeli Alipowaua Wamisri na kuwaokoa Waisraeli kutoka kwa Farao. Bila Shaka, uthibitisho wa haya makubaliano ulikuwa damu ya mwanakondoo iliyopakwa kwenye linta kupitia kwayo Mungu Alianzisha agano na mwanadamu, moja ambalo ilisemwa kuwa wale wote waliokuwa na damu ya mwanakondoo juu na pembeni mwa viunzi vya mlango walikuwa Waisraeli, walikuwa wateuliwa wa Mungu, na wote wangeokolewa na Yehova (kwa kuwa Yehova wakati ule Alikuwa karibu kuwaua wazaliwa wa kwanza wa kiume wa Misri wote na wazaliwa wa kwanza wa kondoo na ng’ombe). Agano hili lina viwango viwili vya maana. Hakuna mmoja wa watu au wanyama wa Misri angeokolewa na Yehova; Angewaua wazaliwa wa kwanza wa kiume na wazaliwa wa kwanza wa kondoo na ng’ombe wao wote. Kwa hivyo, katika vitabu vingi vya unabii kulitabiriwa kwamba Wamisri wangeadibiwa vikali kutokana na agano la Yehova. Hiki ndicho kiwango cha kwanza cha maana. Yehova Aliwaua wazaliwa wa kwanza wa kiume wa Misri na wazaliwa wa kwanza wa mifugo wao wote, na kuwaacha Waisraeli wote, jambo lililomaanisha kuwa wale wote waliokuwa wa nchi ya Israeli walipendwa na Yehova na wote wangeokolewa; Alidhamiria kufanya kazi ya muda mrefu ndani yao, na Alianzisha agano nao kwa kutumia damu ya mwanakondoo. Tangu wakati ule kuendelea, Yehova Asingewaua Waisraeli na Alisema kuwa daima wangekuwa wateuliwa Wake. Angeianza kazi Yake ya Enzi Nzima ya Sheria Miongoni mwa makabila kumi na mawili ya Israeli, Angeziweka wazi sheria Zake zote kwa Waisraeli, na kuchagua manabii na waamuzi kutoka kati yao, na wangekuwa katikati ya kazi Yake. Alifanya Agano nao: Angefanya kazi tu miongoni mwa wateuliwa isipokuwa enzi ibadilike. Agano la Yehova lilikuwa lisilobadilika kwani lilitengenezwa kwa damu, na lilianzishwa na wateuliwa Wake. La muhimu zaidi, Alikuwa Ameteua mawanda na malengo yafaayo ya kazi Yake katika enzi nzima, na kwa hivyo watu waliliona agano kuwa la umuhimu sana. Hiki ndicho kiwango cha pili cha maana ya agano. Isipokuwa kitabu cha Mwanzo, ambacho kilikuwepo kabla ya kuanzishwa kwa agano, vitabu vingine vyote vya Agano la Kale vinaeleza kuhusu kazi miongoni mwa Waisraeli baada ya kuanzishwa kwa agano hili. Bila shaka, yapo maelezo ya hapa na pale ya Watu wa Mataifa, ila kwa ujumla, Agano la Kale linaeleza kuhusu kazi ya Mungu nchini Israeli. Kwa sababu ya Agano kati ya Yehova na Waisraeli, vitabu vilivyoandikwa katika Enzi ya Sheria vinaitwa "Agano la Kale." Vimepatiwa jina hili kutokana na agano la Yehova na Waisraeli.
kutoka kwa "Kuhusu Biblia (2)" katika Neno Laonekana katika Mwili
9. Agano Jipya lilipatiwa jina hilo kutokana na damu iliyomwagwa na Yesu msalabani na agano Lake na wale wote waliomwamini. Agano la Yesu lilikuwa hili: Watu hawakuwa na budi kumwamini ili dhambi zao zisamehewe kwa kumwagika kwa damu Yake, na kwa njia hiyo wangeokolewa na kuzaliwa upya kupitia Kwake, na kamwe wasingeendelea kuwa wenye dhambi; watu walipaswa kumwamini ili wapokee neema Yake, na hawangeteseka jehanamu baada ya kufa. Vitabu vyote vilivyoandikwa wakati wa Enzi ya Neema vilizuka baada ya hili agano, na vyote vinaeleza kuhusu kazi na matamshi yaliyomo. Havielezi zaidi ya wokovu wa kusulubishwa kwa Bwana Yesu au hili agano; vyote ni vitabu vilivyoandikwa na wapendwa katika Bwana waliokuwa na tajriba. Kwa hivyo hivi vitabu vilevile vimepatiwa jina kutokana na agano: Vinaitwa Agano Jipya. Haya Maagano mawili yanajumuisha tu Enzi ya Neema na Enzi ya Sheria na hayana uhusiano na enzi ya mwisho. Hivyo basi, Biblia haina msaada mkubwa kwa watu wa leo wa siku za mwisho. Zaidi, hutumika kama marejeleo ya muda mfupi, ila kimsingi haina matumizi ya thamani kubwa.
kutoka kwa "Kuhusu Biblia (2)" katika Neno Laonekana katika Mwili
10. Sio kila kitu katika Biblia ni rekodi ya maneno aliyoyasema Mungu. Kimsingi Biblia inaandika hatua mbili za awali za kazi ya Mungu, ambapo sehemu moja ni rekodi ya utabiri wa kale wa manabii, na sehemu nyingine ni uzoefu na maarifa yaliyoandikwa na watu waliotumiwa na Mungu katika enzi zote. Uzoefu wa kibinadamu umetiwa doa na maoni na maarifa ya kibinadamu, kitu ambacho hakiepukiki. Katika vitabu vingi vya Biblia kuna dhana nyingi za kibinadamu, upendelevu wa kibinadamu, na ufasiri wa ajabu wa kibinadamu. Ni kweli, maneno mengi ni matokeo ya kupatiwa nuru na kuangaziwa na Roho Mtakatifu, na ni tafsiri sahihi—lakini haiwezi kusemwa kuwa ni udhihirishaji sahihi kabisa wa ukweli. Maoni yao juu ya vitu fulani si chochote zaidi ya maarifa uzoefu binafsi, au kupatiwa nuru na Roho Mtakatifu. Utabiri wa manabii ulikuwa umetolewa na Mungu mwenyewe: Unabii wa Isaya, Danieli, Ezra, Yeremia, na Ezekieli, ulitoka moja kwa moja kwa Roho Mtakatifu, watu hawa walikuwa ni waonaji maono, walipokea Roho ya Unabii, wote walikuwa ni manabii wa Agano la Kale. Wakati wa Enzi ya Sheria watu hawa, ambao walikuwa wamepokea ufunuo wa Yehova, walizungumza unabii mwingi, ambao ulisemwa na Yehova moja kwa moja. Na kwa nini Yehova alifanya kazi ndani yao? Kwa sababu watu wa Israeli walikuwa ni wateule wa Mungu: Kazi ya manabii ilipaswa kufanyika miongoni mwao, na walikuwa wamefuzu kupokea maono hayo. Kimsingi, wao wenyewe hawakuelewa ufunuo wa Mungu kwao. Roho Mtakatifu Alizungumza maneno hayo kupitia vinywa vyao ili watu wa baadaye waweze kuelewa mambo hayo, na kuona kwamba ni kweli ilikuwa ni kazi ya Roho wa Mungu, ya Roho Mtakatifu, na haikutoka kwa mwanadamu, na kuweza kuwathibitishia kazi ya Roho Mtakatifu.
kutoka kwa "Kuhusu Biblia (3)" katika Neno Laonekana katika Mwili
11. Leo, watu wanaamini kwamba Biblia ni Mungu, na kwamba Mungu ni Biblia. Na hivyo pia, wanaamini kwamba maneno yote ya Biblia ni maneno pekee ambayo Mungu alizungumza, na kwamba yote yalizungumzwa na Mungu. Wale wanaomwamini Mungu hata wanafikia hatua ya kufikiri kwamba ingawa vitabu vyote sitini na sita vya Agano la Kale na Agano Jipya viliandikwa na watu, vyote viliandikwa kwa uvuvio wa Mungu, na ni rekodi ya matamshi ya Roho Mtakatifu. Hii ni tafsiri ya watu yenye makosa, na haiafikiani kabisa na kweli. Kimsingi, mbali na vitabu vya unabii, sehemu kubwa ya Agano la Kale ni rekodi ya kihistoria. Baadhi ya nyaraka za Agano Jipya zinatokana na uzoefu wa watu, na baadhi zinatokana na kupatiwa nuru na Roho Mtakatifu; nyaraka za Paulo, kwa mfano, zilitokana na kazi ya mwanadamu, zote zilitokana na kupatiwa nuru na Roho Mtakatifu, na ziliandikwa kwa ajili ya makanisa, yalikuwa ni maneno ya kushawishi na kutia moyo kwa kaka na dada wa makanisa. Hayakuwa maneno yaliyozungumzwa na Roho Mtakatifu—Paulo asingeweza kuzungumza kwa niaba ya Roho Mtakatifu, na wala hakuwa nabii, achilia mbali kuona maono. Nyaraka zake ziliandikwa kwa ajili ya makanisa ya Efeso, Filadefia, Galatia, na makanisa mengineyo. Na hivyo, nyaraka za Paulo za Agano Jipya ni nyaraka ambazo Paulo aliandika kwa ajili ya makanisa, na sio uvuvio wa Roho Mtakatifu, wala sio matamshi ya moja kwa moja ya Roho Mtakatifu. Ni maneno tu ya kushawishi, faraja, na kutia moyo ambayo aliyaandika kwa ajili ya makanisa wakati wa kazi yake. Na hivyo pia, ni rekodi zaidi ya kazi na muda ya Paulo. Ziliandikwa kwa ajili ya kaka na dada wote katika Bwana, na zilikuwa ni kwa ajili ya kuwafanya kaka na dada wa makani yote ya wakati huo kufuata ushauri wake na kudumu siku zote katika njia zote za Bwana Yesu. Kwa namna yoyote ile Paulo hakusema kuwa, iwe ni kwa makanisa ya wakati huo au makanisa ya wakati ujao, yote yanapaswa kula na kunywa vitu vyake, wala hakusema kwamba maneno yake yote yalitoka kwa Mungu. Kulingana na mazingira ya kanisa wakati huo, aliwasiliana tu na kaka na dada, na aliwashawishi, na akawaimarisha imani kwao; na aliwahubiria na kuwakumbusha watu na kuwashawishi. Maneno yake yalijikita katika mzigo wake mwenyewe, na aliwasaidia watu kupitia maneno haya. Alifanya kazi ya mitume wa kanisa wa wakati huo, alikuwa mfanyakazi ambaye alitumiwa na Bwana Yesu, na hivyo alipewa jukumu la makanisa, alipewa jukumu la kufanya kazi ya makanisa, alipaswa kujifunza kuhusu hali za ndugu—na kwa sababu hii, aliandika nyaraka kwa kaka na dada wote katika Bwana. Yote aliyoyasema yale yaliyokuwa ni ya kuadilisha na mazuri kwa watu yalikuwa sahihi, lakini hayakuwa yanawakilisha matamshi ya Roho Mtakatifu, na hakuwa anamwakilisha Mungu. Ni uelewa mbaya kupita kiasi, na makufuru makubwa sana kwa watu kuchukulia rekodi za uzoefu wa mwanadamu na nyaraka za mwanadamu kama maneno yaliyozungumzwa na Roho Mtakatifu kwa makanisa! Hiyo ni kweli kabisa tunapokuja katika nyaraka ambazo Paulo aliziandika kwa ajili ya makanisa, maana nyaraka zake ziliandikwa kwa ajili ya kaka na dada kulingana na mazingira na hali ya kila kanisa kwa wakati huo, na yalikuwa ni kwa ajili ya kuwashawishi kaka na dada katika Bwana, ili waweze kupokea neema ya Bwana Yesu. Nyaraka zake zilikuwa ni kwa ajili ya kuwaamsha kaka na dada wa wakati huo. Inaweza kusemwa kuwa huu ulikuwa ni mzigo wake mwenyewe, na pia ulikuwa ni mzigo aliopewa na Roho Mtakatifu; hata hivyo, alikuwa ni mtume aliyeyaongoza makanisa ya wakati huo, ambaye aliandika nyaraka kwa ajili ya makanisa na kuwashawishi, huo ulikuwa wajibu wake. Utambulisho wake ulikuwa tu ni mtume anayefanya kazi, na alikuwa ni mtume tu aliyetumwa na Mungu; hakuwa mtabiri, wala mtoa unabii. Kwa hivyo kwake, kazi yake mwenyewe na maisha ya kaka na dada yalikuwa na umuhimu mkubwa sana. Hivyo, asingeweza kuzungumza kwa niaba ya Roho Mtakatifu. Maneno yake hayakuwa maneno ya Roho Mtakatifu, wala yasingesemwa kuwa ni maneno ya Mungu, maana Paulo hakuwa chochote zaidi ya kiumbe wa Mungu, na hakika hakuwa Mungu aliyepata mwili. Utambulisho wake haukuwa sawa na ule wa Yesu. Maneno ya Yesu yalikuwa ni maneno ya Roho Mtakatifu, yalikuwa ni maneno ya Mungu, maana utambulisho wake ulikuwa ule wa Kristo—Mwana wa Mungu. Inawezekanaje Awe sawa na Paulo? Ikiwa watu wanaona nyaraka au maneno kama ya Paulo kama matamshi ya Roho Mtakatifu, na kuwaabudu kama Mungu, basi inaweza kusemwa tu kuwa ni watu wasiochagua kwa busara. Tukisema kwa ukali zaidi, haya sio makufuru? Inawezekanaje mwanadamu azungumze kwa niaba ya Mungu? Na inawezekanaje watu wapigie magoti rekodi za nyaraka zake na maneno aliyoyazungumza kana kwamba yalikuwa ni kitabu kitakatifu, au kitabu cha mbinguni? Je, inawezekana maneno ya Mungu kutamkwa kwa kawaida na mwanadamu? Inawezekanaje mwanadamu azungumze kwa niaba ya Mungu? Na hivyo, unasemaje—kwamba nyaraka alizoandika kwa ajili ya makanisa haziwezi kutiwa doa na mawazo yake mwenyewe? Inawezekanaje zisitiwe doa na mawazo ya kibinadamu? Aliandika nyaraka kwa ajili ya makanisa kulingana na uzoefu wake binafsi, na kiwango cha maisha yake binafsi. Kwa mfano, Paulo aliandika waraka kwa kanisa la Wagalatia ambao ulikuwa na maoni fulani, na Petro aliandika waraka mwingine, ambao ulikuwa na mtazamo mwingine. Ni upi kati ya hizo ulitoka kwa Roho Mtakatifu? Hakuna anayeweza kutoa jibu, hakika. Hivyo inaweza kusemwa tu kwamba wote wanawiwa na mzigo kwa makanisa, lakini barua zao zinawakilisha kimo chao, zinawakilisha vile wanavyowapatia na kuwasaidia kaka na dada, na vile wanavyowiwa na makanisa, na zinawakilisha tu kazi ya binadamu; hayakuwa ya Roho Mtakatifu kabisa. Ikiwa unasema kwamba nyaraka zake ni maneno ya Roho Mtakatifu, basi wewe ni mpumbavu, na unafanya makufuru! Nyaraka za Paulo na nyaraka nyingine za Agano Jipya ni sawa na kumbukumbu za viongozi mashuhuri wa kiroho wa hivi karibuni. Zipo sawa na vitabu vya Watchman Nee au uzoefu wa Lawrence, na kadhalika. Ni vile tu vitabu vya viongozi mashuhuri wa kiroho wa hivi karibuni havijajumuishwa katika Agano Jipya, lakini hulka ya watu hawa ni sawa: Kulikuwa na watu ambao walitumiwa na Roho Mtakatifu wakati fulani, na hawakuweza kumwakilisha Mungu moja kwa moja.
kutoka kwa "Kuhusu Biblia (3)" katika Neno Laonekana katika Mwili
12. Injili ya Mathayo ya Agano Jipya inaandika ukoo wa Yesu. Mwanzoni, inasema kwamba Yesu alikuwa mzao wa Abrahamu, mwana wa Daudi, na mwana wa Yusufu; sehemu inayofuata inasema kwamba Yesu alizaliwa kwa njia ya Roho Mtakatifu, na kuzaliwa na bikira—kitu kinachomaanisha kwamba Hakuwa mwana wa Yusufu au mzao wa Abrahamu, kwamba Hakuwa mwana wa Daudi. Hata hivyo, orodha ya ukoo inasisitiza kumhusisha Yesu na Yusufu. Sehemu inayofuata, orodha ya ukoo inaanza kurekodi mchakato ambao kwa huo Yesu alizaliwa. Inasema mimba ya Yesu ilitungwa kwa njia ya Roho Mtakatifu, kwamba Alizaliwa na bikira, na sio mwana wa Yusufu. Lakini katika orodha ya ukoo imeandikwa waziwazi kwamba Yesu alikuwa mwana wa Yusufu, na kwa kuwa orodha ya ukoo iliandikwa kwa ajili ya Yesu, inaandika vizazi arobaini na mbili. Inapokwenda katika ukoo wa Yusufu, inasema kwa haraka kwamba Yusufu alikuwa mume wa Mariamu, haya ni maneno kwa ajili ya kuthibitisha kwamba Yesu alikuwa mzao wa Abrahamu. Je, huu si mkanganyiko? Orodha hii ya ukoo inaonyesha waziwazi chimbuko la Yusufu, ni wazi kwamba hii ni orodha ya ukoo wa Yusufu, lakini Mathayo anasisitiza kwamba ni orodha ya ukoo wa Yesu. Je, hii haipingi ukweli kwamba Yesu alizaliwa kwa njia ya Roho Mtakatifu? Hivyo, orodha ya ukoo iliyoandikwa na Mathayo sio mawazo ya kibinadamu? Hii ni dhihaka! Kwa namna hii, unaweza kujua kwamba kitabu hiki sio chote kimetoka kwa Roho Mtakatifu. Pengine, kuna baadhi ya watu wanaodhani kwamba Mungu lazima atakuwa na orodha ya ukoo duniani, na matokeo yake ni kwamba wanampachika Yesu kama kizazi cha arobaini na viwili cha Abrahamu. Hii ni dhihaka kabisa! Baada ya kuja duniani, Mungu angewezaje kuwa na orodha ya ukoo? Ikiwa unasema kwamba Mungu ana ukoo, je, humweki katika madaraja sawa miongoni mwa viumbe wa Mungu? Maana Mungu si wa ulimwengu, Yeye ni Bwana wa uumbaji, na ingawa yeye ni wa mwili, hana asili sawa na mwanadamu. Unawezaje kumweka Mungu katika daraja sawa na viumbe wa Mungu? Abrahamu hawezi kumwakilisha Mungu; alikuwa ni mhusika wa kazi ya Yehova wakati huo, alikuwa ni mtumishi mwaminifu tu aliyethibitishwa na Yehova, na alikuwa mmoja wa watu wa Israeli. Inawezekanaje awe babu wa Yesu?
kutoka kwa "Kuhusu Biblia (3)" katika Neno Laonekana katika Mwili
13. Vitabu vya injili ya Agano Jipya vilirekodiwa miaka ishirini hadi thelathini baada ya Yesu kusulubiwa msalabani. Kabla ya hapo, watu wa Israeli walisoma tu Agano la Kale. Hiyo ni sawa na kusema, katika Enzi ya Neema watu walisoma Agano la Kale. Agano Jipya lilionekana tu wakati wa Enzi ya Neema. Agano Jipya halikuwepo wakati wa kazi ya Yesu; watu waliandika kazi Yake baada ya kuwa amefufuka na kupaa mbinguni. Baada ya hapo kulikuwa na Injili Nne, katika nyongeza hiyo pia kulikuwa na nyaraka za Paulo na Petro, na vile vile kitabu cha Ufunuo. Zaidi ya miaka mia moja tu baada ya Yesu kupaa mbinguni, ambapo vizazi vilivyofuata vilipangilia rekodi zao, na kuzaliwa Agano Jipya. Ni baada tu ya kazi hii kukamilika ndipo kukapatikana Agano Jipya; halikuwepo hapo kabla. Mungu alikuwa amefanya kazi yote hiyo, mtume Paulo alifanya kazi yote hiyo, na baadaye nyaraka za Paulo na Petro ziliunganishwa, na njozi kuu zaidi iliyorekodiwa na Yohana katika kisiwa cha Patmo iliwekwa mwishoni, maana ilikuwa inatoa unabii wa kazi ya siku za mwisho. Hii yote ilikuwa ni mipango ya vizazi vilivyofuata na ni tofauti na matamshi ya leo. Kile kilichorekodiwa leo ni kulingana na hatua za kazi ya Mungu; kile ambacho watu wanashughulika nacho leo ni kazi ambayo imefanywa na Mungu Mwenyewe, na maneno yaliyotamkwa na Mungu Mwenyewe. Hupaswi kuingilia—maneno, ambayo yanatoka moja kwa moja kwa Roho Mtakatifu, yamepangwa hatua kwa hatua, na ni tofauti na mpangilio wa rekodi za wanadamu. Inaweza kusemwa kuwa, kile walichorekodi kilikuwa ni kulingana na kiwango chao cha elimu na tabia. Kile walichokirekodi kilikuwa ni uzoefu wa wanadamu, na kila mmoja alikuwa na namna yake ya kurekodi na kuelewa, na kila rekodi ilikuwa tofauti. Hivyo, ikiwa unaiabudu Biblia kama Mungu wewe ni mjinga na mpumbavu wa kutupwa! Kwa nini usitafute kazi ya Mungu wa leo? Ni kazi ya Mungu tu ndiyo inayoweza kumwokoa mwanadamu. Biblia haiwezi kumwokoa mwanadamu, haijabadilika kabisa kwa maelfu ya miaka, na kama unaiabudu Biblia hutaweza kupata kazi ya Roho Mtakatifu.
kutoka kwa "Kuhusu Biblia (3)" katika Neno Laonekana katika Mwili
14. Watu wengi wanaamini kwamba kuelewa na kuwa na uwezo wa kufasiri Biblia ni sawa na kutafuta njia ya kweli—lakini, kimsingi, je, vitu ni rahisi sana? Hakuna anayejua uhalisia wa Biblia: kwamba si kitu chochote zaidi ya rekodi ya kihistoria ya kazi ya Mungu, na agano la hatua mbili zilizopita za kazi ya Mungu, na haikupatii ufahamu wa malengo ya kazi ya Mungu. Kila mtu ambaye amesoma Biblia anajua kwamba inarekodi hatua mbili za kazi ya Mungu wakati wa Enzi ya Sheria na Enzi ya Neema. Agano la Kale linaandika historia ya Israeli na kazi ya Yehova kuanzia wakati wa uumbaji hadi mwisho wa Enzi ya Sheria. Agano Jipya linarekodi kazi ya Yesu duniani, ambayo ipo katika Injili Nne, vilevile kazi ya Paulo; je, sio rekodi za kihistoria? Kuleta mambo ya zamani leo kunayafanya yawe historia, haijalishi yana ukweli kiasi gani, bado ni historia—na historia haiwezi kushughulikia masuala ya leo. Maana Mungu haangalii historia! Na hivyo, kama unaelewa tu Biblia, na huelewi chochote kuhusu kazi ambayo Mungu anakusudia kufanya leo, na kama unamwamini Mungu, na hutafuti kazi ya Roho Mtakatifu, basi hujui inamaanisha nini kumtafuta Mungu. Ikiwa unasoma Biblia kwa lengo la kujifunza historia ya Israeli, kutafiti historia ya uumbaji wa Mungu wa mbingu na dunia, basi humwamini Mungu. Lakini leo, kwa kuwa unamwamini Mungu, na kutafuta uzima, kwa kuwa unatafuta maarifa juu ya Mungu, na hutafuti nyaraka na mafundisho mfu, au ufahamu wa historia, unapaswa kutafuta mapenzi ya Mungu ya leo, na unapaswa kutafuta uongozi wa kazi ya Roho Mtakatifu. Kama ungekuwa mwanaakiolojia ungeweza kusoma Biblia—lakini wewe sio mwanaakiolojia, wewe ni mmoja wa wale wanaomwamini Mungu, na utakuwa bora zaidi ukitafuta mapenzi ya Mungu ya leo.
kutoka kwa "Kuhusu Biblia (4)" katika Neno Laonekana katika Mwili
15. Biblia ni rekodi ya kihistoria ya kazi ya Mungu katika Israeli, na inaandika utabiri mwingi wa manabii wa kale vilevile baadhi ya matamshi ya Yehova katika kazi Yake wakati huo. Hivyo, watu wote wanakitazama kitabu hiki kama kitakatifu (maana Mungu ni mtakatifu na mkuu). Kimsingi, hii yote ni matokeo ya uchaji wao kwa Yehova na vile walivyokuwa wanampenda Mungu. Watu wanarejelea kitabu hiki kwa namna hii kwa sababu tu viumbe wa Mungu wanamwabudu sana Muumba wao, na hata kuna wale ambao wanakiita kitabu hiki kitabu cha mbinguni. Kimsingi, ni rekodi tu za kibinadamu. Hakikupewa jina na Yehova Mwenyewe, wala Yehova Mwenyewe hakuongoza utengenezaji wake. Kwa maneno mengine, mwandishi wa kitabu hiki sio Mungu, bali ni wanadamu. Biblia Takatifu ni jina la heshima tu lililotolewa na mwanadamu. Jina hili halikuamuliwa na Yehova na Yesu baada ya kujadiliana; si chochote zaidi ya mawazo ya kibinadamu. Maana kitabu hiki hakikuandikwa na Yehova, wala kuandikwa na Yesu. Badala yake, ni maelezo ya manabii wengi wa kale, mitume na waonaji maono, ambayo baadaye yalipangiliwa na vizazi vilivyofuata na kuwa kitabu cha maandiko ya kale, ambayo kwa watu, yanaonekana kuwa matakatifu, kitabu ambacho wanaamini kimejumuisha siri nyingi ambazo hazieleweki na za kina ambazo zinasubiri kufunguliwa na vizazi vijavyo. Kwa namna hiyo, watu hata wanaamini kwamba kitabu hiki ni kitabu cha mbinguni. Ukijumlisha Injili Nne na Kitabu cha Ufunuo, mtazamo wa watu kuhusu kitabu hicho ni tofauti kabisa na vitabu vingine, na hivyo hakuna mtu anayethubutu kukichambua hiki kitabu cha mbinguni—kwa sababu ni kitakatifu sana.
kutoka kwa "Kuhusu Biblia (4)" katika Neno Laonekana katika Mwili
16. Leo, Ninaichambua Biblia kwa namna hii na haimaanishi kwamba Naichukia, au kukana thamani yake kwa ajili ya marejeleo. Ninakuelezea thamani ya asili na asili ya Biblia ili uweze kuondoka katika giza. Maana watu wana mitazamo mingi kuhusu Biblia, na mingi yao ina makosa; kusoma Biblia kwa namna hii sio tu kunawazuia kupata kile wanachopaswa kupata, lakini, muhimu zaidi, kunazuia kazi Niliyokusudia kufanya. Ni kero kubwa kwa kazi ya siku zijazo, na inatoa hasara tu, na wala sio faida. Hivyo, Ninachokufundisha ni hulka tu na kisa cha ndani cha Biblia. Sikwambii kwamba usisome Biblia, au uzunguke ukitangaza kwamba haina thamani kabisa, bali kwamba uweze kuwa na maarifa na mtazamo sahihi juu ya Biblia. Usiegemee upande mmoja sana! Ingawa Biblia ni kitabu cha historia kilichoandikwa na wanadamu, pia kinaandika kanuni nyingi ambazo kwazo watakatifu wa zamani na manabii walimhudumia Mungu, vilevile uzoefu wa hivi karibuni wa mitume katika kumhudumia Mungu—yote haya yalishuhudiwa na kujulikana kwa watu hawa, na inaweza kutumika kama rejeleo kwa ajili ya watu wa enzi hii katika kutafuta njia ya kweli. Hivyo, katika kusoma Biblia watu wanaweza pia kupata njia nyingi za maisha ambazo haziwezi kupatikana katika vitabu vingine. Njia hizi ni njia za maisha ya kazi ya Roho Mtakatifu ambazo manabii na mitume walizipitia katika enzi iliyopita, na maneno mengi ni ya thamani, na yanaweza kutoa kile ambacho watu wanataka. Hivyo, watu wote wanapenda kusoma Biblia. Kwa sababu kuna mambo mengi sana yaliyofichwa katika Biblia, mitazamo ya watu juu ya Biblia ni tofauti na mitazamo yao juu ya maandiko ya viongozi wa kiroho mashuhuri. Biblia ni rekodi na mkusanyiko wa uzoefu na maarifa ya watu ambao walimhudumia Yehova na Yesu katika enzi ya kale na mpya, na pia vizazi vya baadaye vimeweza kupata nuru, mwanga mkubwa na njia za kuweza kutembea kwazo. Sababu ya Biblia kuwa na hadhi ya juu kuliko maandiko ya kiongozi yeyote mkubwa wa kiroho ni kwa sababu maandiko yao yote yanatoka katika Biblia, uzoefu wao wote unatokana na Biblia, na wote wanaelezea Biblia. Na hivyo, ingawa watu wanaweza wakafaidika na vitabu kutoka kwa kiongozi yeyote wa kiroho mashuhuri, bado wanaiabudu Biblia, maana kwao, inaonekana ni ya juu sana na ya kina sana! Ingawa Biblia inaleta pamoja baadhi ya vitabu vya maneno ya uzima, kama vile nyaraka za Paulo na nyaraka za Petro, na ingawa watu wanaweza kusaidiwa na vitabu hivi, vitabu hivi bado vimepitwa na wakati, bado ni vitabu vya enzi ya kale, na haijalishi ni vizuri kiasi gani, vinafaa tu kwa ajili ya kipindi kimoja, na wala sio vya milele. Maana kazi ya Mungu siku zote inaendelea, na haiwezi kusimama tu katika kipindi cha Paulo na Petro, au siku zote ibaki katika Enzi ya Neema, enzi ambayo Yesu alisulubiwa. Na hivyo, vitabu hivi vinafaa tu katika Enzi ya Neema, na wala sio kwa ajili ya Enzi ya Ufalme wa siku za mwisho. Vinaweza tu kuwa na manufaa kwa waumini wa Enzi ya Neema, na sio kwa watakatifu wa Enzi ya Ufalme, na haijalishi ni vizuri kiasi gani, bado havifai kwa kipindi hiki. Ni sawa na kazi ya Yehova ya uumbaji au kazi Yake katika Israeli: Haijalishi kazi hii ilikuwa kubwa kiasi gani, bado imepitwa na wakati, na muda utaendelea kuja wakati umekwishapita. Kazi ya Mungu pia ni ile ile: Ni nzuri, lakini muda utafika ambapo itakoma; siku zote haitaendelea kubaki katikati ya kazi ya uumbaji, wala katikati ya kazi ile ya msalaba. Haijalishi kazi ya msalaba inashawishi kiasi gani, haijalishi ilikuwa ni fanisi kiasi gani katika kumshinda Shetani, hata hivyo, kazi bado ni kazi, na enzi, hata hivyo bado ni enzi; kazi siku zote haiwezi kubaki katika msingi ule ule, wala nyakati haziwezi kukosa kubadilika, kwa sababu kulikuwa na uumbaji na lazima kuwepo na siku za mwisho. Hii haiepukiki! Hivyo, leo maneno ya uzima katika Agano Jipya—nyaraka za mitume, na Injili Nne—vimekuwa vitabu vya kihistoria, vimekuwa vitabu vya kale, na inawezekanaje vitabu vya kale kuwapeleka watu katika enzi mpya? Haijalishi ni kiasi gani vitabu hivi vinaweza kuwapatia watu uzima, haijalishi vina uwezo kiasi gani katika kuwaongoza watu kwenye msalaba, ndio kwamba havijapitwa na wakati? Havijaondokewa na thamani? Hivyo, Ninasema hupaswi kuviamini vitabu hivi bila kufikiri. Ni vya zamani sana, haviwezi kukupeleka katika kazi mpya, vinaweza kukulemea tu. Sio tu haviwezi kukuleta katika kazi mpya, na katika kuingia kupya, bali vinakupeleka katika makanisa ya dini ya kale na kama ni hivyo, havirudishi nyuma imani yako kwa Mungu?
kutoka kwa "Kuhusu Biblia (4)" katika Neno Laonekana katika Mwili
17. Ili kuielewa Biblia, kuelewa historia, bali sio kuelewa kile ambacho Roho Mtakatifu anafanya leo—hayo ni makosa! Umefanya vizuri sana katika kujifunza historia, umefanya kazi nzuri sana, lakini huelewi chochote juu ya kazi Anayofanya Roho Mtakatifu leo. Je, huu si upumbavu? Watu wengine wanakuuliza: "Mungu anafanya nini leo? Ni kitu gani unapaswa kuingia kwacho leo? Maisha yako yanakwendaje? Je, unaelewa mapenzi ya Mungu?" Hutakuwa na majibu ya kile wanachouliza—sasa unajua nini kwani? Utasema: Ninajua tu kwamba ninapaswa kupuuzia mambo ya mwili na kujitambua. Halafu wakiuliza tena "Ni kitu gani kingine ambacho unakielewa?" Utasema unajua pia kutii mipangilio yote ya Mungu, na kujua kidogo kuhusu historia ya Biblia, basi. Hicho tu ndicho umepata kwa kumwamini Mungu miaka yote hii? Ikiwa hayo tu ndiyo unayoyaelewa, basi unapungukiwa mengi sana.
kutoka kwa "Kuhusu Biblia (4)" katika Neno Laonekana katika Mwili
kutoka kwa Neno Laonekana katika Mwili
Kujua zaidi: Asili ya Kanisa la Mwenyezi Mungu, Umeme wa Mashariki Hutoka wapi?

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni